KAMBI YAKE YAPETA UWT, SASA WAJIPANGA UVCCM, WAZAZI
KAMBI
 ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa imeendelea kuyanyanyasa 
makundi mengine ndani ya CCM, ambayo yamekuwa yakijipanga kwa ajili ya 
Uchaguzi Mkuu wa 2015.Kambi ya kiongozi huyo ni kama imehamia Dodoma ili
 kuhakikisha watu wake wanashinda katika chaguzi za viongozi wa juu wa 
jumuiya za CCM baada ya kufanikisha kile inachodai kuwa ushindi mkubwa 
katika ngazi za wilaya na mkoa kutokana na watu wake wengi kushinda.
Wapambe
 wa Lowassa wakiongozwa na Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba na 
Mjumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UVCCM), Hussein Bashe wapo 
Dodoma kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu wa uchaguzi wa Jumuiya ya 
Wanawake (UWT) na wataendelea kuwapo mpaka jumuiya zote zitakapokuwa 
zimefanya uchaguzi huo.
“Hapa kazi ni moja tu, hakuna kulala 
maana tukilala tutajikuta tumewekwa pabaya. Tumefanikiwa UWT na sasa 
tunaelekeza majeshi yetu UVCCM... lazima tuhakikishe tunakomesha uonevu 
wa kuitana magamba mwaka huu,” alisema mmoja wa wapambe wa Lowassa juzi 
usiku.
Matokeo ya uongozi wa juu wa UWT yameongeza matumaini kwa 
kambi hiyo ambayo imezoa zaidi ya asilimia 80 ya viongozi katika jumuiya
 hiyo yenye ushawishi mkubwa katika uamuzi mbalimbali wa chama hicho.
Mwenyekiti
 wa UWT Taifa, Sophia Simba ambaye alitetea vizuri nafasi yake na Makamu
 wake, Asha Bakari Makame wanatajwa kuwa katika kambi hiyo huku wajumbe 
saba kati ya tisa waliochaguliwa kuiwakilisha jumuiya hiyo katika 
Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ya chama hicho, wakiwa waumini wa kambo 
hiyo.
Walioshinda nafasi za ujumbe wa NEC ambao wanatajwa kuwa 
wafuasi wa Lowassa ni pamoja na Mbunge wa Ukonga, Eugen Mwaiposa, Waziri
 wa zamani wa Maliasili na Utalii, Shamsa Mwangunga na Mwenyekiti wa 
Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, Pindi Chana.
Wengine ni wabunge wa Viti Maalumu, Diana Chilolo, Zainabu Kawawa, Mary Mwanjelwa na Subira Mgalu. 
Wajumbe
 wawili ambao ni pamoja na Naibu Waziri wa Fedha, Janeth Mbene yeye 
anatajwa kuwa hana kundi lolote wakati Mbunge wa Viti Maalumu, Betty 
Machangu ambaye anatajwa kwamba alikuwa akimuunga mkono Mbunge wa Same 
Mashariki, Anna Kilango Malecela.
Kilango ambaye alikuwa akiungwa
 mkono na makundi ya watu waliojipambanua kuwa wapambanaji na ufisadi, 
aliangushwa vibaya na Simba kwa zaidi ya kura 400 katika kinyang’anyiro 
cha nafasi ya Mwenyekiti wa UWT.
Vigogo wengine wanaotajwa kuwa na 
kambi katika kinyang’anyiro hicho cha urais wa 2015 ni Waziri wa Mambo 
ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe na Waziri wa 
Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta ambao katika uchaguzi wa 
jumuiya za CCM nguvu zao zinaonekana kuwa si kubwa kama ilivyotarajiwa.
JK awapasha viongozi UWT
Mwenyekiti
 wa CCM, Rais Jakaya Kikwete juzi usiku aliwatolea uvivu viongozi wa 
UWT, akiwataka kuchukua hatua za kumaliza nyufa zilizosababishwa na 
uchaguzi uliomalizika Jumamosi iliyopita.
Rais Kikwete alisema 
viongozi waliochaguliwa wakiongozwa na Simba ambaye pia Waziri wa 
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto wachukue hatua kuondoa makundi 
ambayo yanatokana na uchaguzi.
“Hii jumuiya siyo yenu, ni ya 
wanachama kwa hiyo baada ya uchaguzi lazima muwe tayari kufanya kazi na 
kila mmoja, isije ikawa ni wale marafiki zako tu maana ikiwa hivyo 
utamteua hata kama uwezo hana,” alisema Kikwete alipokuwa akifunga 
mkutano huo wa uchaguzi mjini Dodoma.
Alikemea tabia ya chuki 
inayojengwa na uchaguzi akisema inatokana na viongozi walioko katika 
nafasi mbalimbali za uongozi kudhani kwamba wanazimiliki binafsi.
“Hupaswi
 kumchukia mtu eti kwa sababu amegombea nafasi fulani, hakuna nafasi ya 
mtu, nafasi zote ni za chama, kwa hiyo kama ulikuwa mwenyekiti, uongozi 
wako unakoma pale tunapotangaza upya uchaguzi,” alisema Rais Kikwete na 
kuongeza:
“Tukishatangaza kila mwanachama mwenye sifa anakuwa na 
haki ya kugombea nafasi hizo, sasa wewe usimchukie na kumuuliza eti kwa 
nini unagombea nafasi yangu, siyo nafasi yako, hii ni nafasi ya chama.”
Alikemea
 tabia ya baadhi ya viongozi au wagombea kuwajengea chuki wale ambao 
hawakuwaunga mkono, na kwamba anayefanya hivyo hapaswi kuwa kiongozi.
Alisema
 kiongozi wa aina hiyo daima ataongoza kwa makundi, akiwapenda wale 
waliomuunga mkono na kuwatenga wale ambao walikuwa na mtazamo tofauti 
jambo ambalo ni hatari kwa ustawi wa jumuiya na chama kwa jumla.
“Kila
 mwanachama ana uhuru wa kumuunga mkono mtu anayempenda, sasa wewe 
unapomkasirikia na kumjengea chuki unamaanisha nini? Demokrasia maana 
yake ni kila mmoja wetu kumchagua mtu anayeona anafaa,” alisema.
Alitoa
 mfano kwamba baada ya yeye kuteuliwa kuwa mgombea wa urais kupitia CCM 
mwaka 2005 na baada ya uchaguzi uliompa ushindi, aliwateua wale 
waliokuwa washindani wake katika Baraza la Mawaziri, akiwamo Waziri wa 
Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya.
“Mwandosya
 tuko naye hadi leo, hata wale waliokuwa wakinipinga na wengine 
walinifanyia mambo ya ajabu kwelikweli, lakini hayo yote inafika mahali 
unaweka kando maana huwezi kuongoza nchi kwa kuwateua marafiki zako tu,”
 alisema Kikwete. 
Uchaguzi UVCCM leo
Rais Kikwete leo 
anatarajia kufungua Mkutano wa Nane wa UVCCM utakaofanyika katika Chuo 
cha Mipango, Dodoma huku vita kubwa ikitarajiwa katika uchaguzi kwa 
misingi ya kambi za urais kuelekea 2015.
Vita kubwa katika uchaguzi 
huo ni katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti ambayo inawaniwa na Paul 
Makonda, Mboni Mhina na Ally Salum Hapi, wakati nafasi ya Mwenyekiti 
inawaniwa na Sadifa Juma Khamis, Rashid Simai Msaraka na Lulu Msham 
Abdallah.
Katika nafasi ya umakamu, Makonda anaungwa mkono na 
kambi ya Membe, wakati kambi ya Lowassa imeamua kuelekeza nguvu zake kwa
 mwanadada, Mboni. Kambi hiyo pia inamuunga mkono Sadifa anayegombea 
nafasi ya Uenyekiti.
Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigela alisema 
jumuiya yake inafuatilia mienendo ya wagombea wote na wapambe wao na 
kwamba watakaobainika kukiuka taratibu za uchaguzi watachukuliwa hatua. 
Akizungumzia
 suala la rushwa ambalo linaonekana kuiandama CCM pamoja na jumuiya 
zake, Shigela alisema: “Katika hilo tumejipanga vizuri kukabiliana 
nalo.”
“Mfano mzuri ni kule Zanzibar, katika Mkoa wa Mjini 
Magharibi tumetengua nafasi za wajumbe wawili wa Baraza, hii ni 
kuonyesha kuwa hatutanii lazima watu wawe waadilifu,” alisema.
Kwa
 mujibu wa Kanuni ya Umoja wa Vijana, mkutano huo utakuwa chini ya 
Uenyekiti wa Benno Malisa kwani kanuni inasema kama mwenyekiti si 
mgombea, basi ndiye atakayeongoza mkutano huo.
Mkutano huo pamoja na kuchagua viongozi wa UVCCM, pia utapitisha katiba mpya ya jumuiya hiyo.
CHANZO: MWANANCHI
 
No comments:
Post a Comment