Wednesday, November 21, 2012


UTAFITI umebaini kuwa sindano za uzazi wa mpango zinachangia kasi ya maambukizi ya virusi vya Ukimwi kwa kuwa zina vichocheo vingi ambavyo vinahuisha virusi vya Ukimwi katika nyumba ya uzazi na kuvipa nguvu ya kusambaa.

Inaelezwa kuwa walio katika hatari zaidi ya maambukizi hayo ni wanawake walioko katika ndoa kwa kuwa ndiyo wanaotumia zaidi sindano hizo.

Utafiti huo uliofanywa na wanasayansi wa Marekani na kuripotiwa na gazeti la The Guardian la Uingereza, umebaini kuwa wanawake wanaotumia sindano za uzazi wa mpango wapo katika hatari mara mbili ya kupata maambukizi ya Ukimwi au kuwaambukiza wenzi wao, kuliko wengine.

Katika utafiti huo uliofanywa katika nchi saba zinazoendelea barani Afrika ikiwamo Tanzania, wanasayansi hao kutoka Chuo Kikuu cha Washington, walipendekeza ushauri zaidi utolewe kwa wanandoa kabla mtu hajajiingiza kwenye matumizi ya sindano kama njia ya kupanga uzazi.

Utafiti huo ulifanyika kwa wanandoa 3,790 kutoka nchi za Tanzania, Afrika Kusini, Zimbabwe, Uganda, Kenya, Rwanda na Botswana, ulichapishwa kwa mara ya kwanza katika Jarida la Afya la Lancet kabla ya kunukuliwa na gazeti la The Guardian.

Utafiti umebaini pia kuwa zaidi ya wanawake 140 milioni duniani wanatumia njia mbalimbali za uzazi wa mpango, huku wanandoa wengi katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, wanaoishi na VVU wakichagua kutumia sindano kama njia ya kuzuia mimba zisizotarajiwa.

Wanasayansi hao walikusanya taarifa kati ya wanandoa 3,790 ambao mmoja wao anaishi na VVU na mwenza wake akiwa hana maambukizo.

Aidha, wanawake ambao wanaishi na VVU na wanatumia sindano hizo pia walikuwa katika hatari zaidi ya kuwaambukiza wenzi wao.

Vipimo vilionyesha kuwa sindano hizo ambazo zina vichocheo ambavyo vinavipa nguvu virusi ndani ya nyumba ya uzazi (cervix).

Imeelezwa kuwa njia za uzazi wa mpango zinazohamasishwa zaidi na kupendwa zaidi na wanawake ni sindano, ambazo wanawake wanasema kuwa zinadumu kwa muda mrefu na zinaweza kutumika bila ya ruhusa au mume kufahamu.

Kiongozi mkuu wa utafiti huo, Renee Heffron wa Chuo Kikuu cha Washington alisema sindano za uzazi wa mpango zina vichocheo vingi ambavyo huvihuisha vijidudu vya Ukimwi katika nyumba ya uzazi na kuvipa nguvu ya kusambaa.

 “Ni vyema sasa kama tutasisitiza njia za uzazi wa mpango ambazo ni salama zaidi kama vile mipira ya kiume au njia nyingine ambazo hazina vichocheo (hormones) au zina kiasi kidogo cha vichocheo,” alisema Dk Heffron.

Mwanasayansi mwingine, Charles Morrison wa Kituo cha Afya cha Durham, nchini Marekani alisema uhamasishaji wa matumizi ya sindano za uzazi wa mpango unachochea maambukizi zaidi katika nchi za Jangwa la Sahara.

“Ushauri wangu kwa nchi zinazoendelea ni kuacha matumizi ya njia za uzazi wa mpango zenye vichocheo, ili tupunguze maambukizi, jibu la tatizo hili linatakiwa litafutwe sasa, nchi zinazohusika zinatakiwa zishiriki katika hili,” alisema.

Alivitaka vituo vya afya vitoe ushauri kwa wanawake kutumia kondomu badala ya sindano au vidonge.

Mara nyingi watu wanaotumia vidonge, wengi si wanandoa, mtu anayemeza vidonge vya kuzuia mimba anaogopa zaidi mimba, si Ukimwi.

Huchoche hamu ya mapenzi

Mfamasia katika Kitengo cha Dawa kwa watu wanaoishina VVU katika Hospitali ya Amana, Christopher Masika alisema anaafiki kuwa sindano na hata vidonge vinaweza kuwa ni sababu inayochochea maambukizi kwa sababu ya uhuru.

“Ninachokiona mimi katika hilo ni uhuru. Mtu anapotumia sindano huwa huru kufanya ngono kwa kuwa hana hofu ya mimba, hicho kinaweza kumfanya apate maambukizi kwa urahisi, tofauti na anapotumia kondomu,” alisema.

Alisema wapo baadhi ambao wakitumia sindano hizo vichocheo vinawafanya wapate hamu zaidi ya kufanya mapenzi, hivyo huanza kutembea na wanaume wengine.

Aliongeza kuwa mtu anayeishi na VVU akizuia mimba kwa njia ya sindano, ni rahisi kupata maambukizi mapya kutoka kwa mwenza wake.

Masika alisema wanawake wapewe elimu zaidi kwani wapo ambao wanadanganywa kuwa njia za uzazi wa mpango kama sindano, povu zinaweza kuzuia maambukizi, jambo ambalo si la kweli.

Wakati huohuo baadhi ya wanandoa wanaoishi na VVU wanaopata matibabu katika Hospitali ya Amana wamesema kuwa tangu waanze kutumia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi (ARVs) hamu ya kufanya mapenzi imeongezeka kwa kasi kubwa.

Mkuu wa Kitengo cha Utafiti cha Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (Tacaids), Dk Arodia Mulokozi, alisema taasisi yake haiwezi kuzungumza lolote kuhusu utafiti huo, badala yake alilitaka Mwananchi kuzungumza na Kitengo cha Afya ya Uzazi wa Mpango cha Muhimbili.

“Hatuhusiki na masuala ya uzazi wa mpango, nafikiri unaweza kuzungumza na Kitengo cha ‘Reproductive Health’ cha Muhimbili,” alisema Dk Mulokozi.

Waziri wa Afya hakupatika, lakini msemaji wa wizara hiyo, Nsachris Mwamwaja alisema ni mapema mno kuchangia kuhusu utafiti huo, atafanya hivyo pindi atakapopata taarifa zaidi.

Mratibu wa Mpango wa  Uzazi wa Mpango Tanzania (Umati), Dk Morris Hiza amekiri kuufahamu utafiti huo, lakini akaeleza kuwa haujajitosheleza na bado una maswali mengi.

“Nilikuwapo wakati Heffron anawasilisha utafiti wake mjini Geneva, lakini nakumbuka mkutano ule wa WHO (Shirika la Afya Duniani) uliukataa,” alisema.

Alieleza kuwa Heffton alifanya utafiti huo kwa nyani na wanawake makahaba pekee.


CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment